shamba-la-mpunga

Kilimo cha Kisasa cha Mpunga

Taarifa muhimu kuhusu zao la mpunga

Mpunga ni zao la pili la chakula kwa umuhimu linalolimwa sehemu nyingi nchini Tanzania. Umuhimu wa zao hili umeongezeka kuanzia muongo uliopita kutokana na jamii za mijini na vijijini kupendelea zaidi kula wali na kupunguza ulaji wa vyakula vingine na kulifanya zao hili kuwa la chakula na biashara.

Mazingira yanayofaa kwa kulima mpunga

Mvua ni chanzo kikuu cha maji kwenye kilimo cha mpunga. Viwango vya mahitaji ya maji katika kukua kwa mpunga hutofautiana miongoni mwa aina za mpunga. Ni kwa jinsi hii mpunga hupandwa katika mazingira mbalimbali kutegemea na mahitaji yake ya maji.

Zipo aina tatu kuu za mazingira yanayolimwa mpunga kulingana na upatikanaji wa maji na hali ya mwinuko wa nchi. Mazingira haya ni kilimo cha mpunga wa mabondeni kinachotegemea mvua (72%), kilimo cha mpunga wa kwenye miinuko (20%) na kilimo cha mpunga cha umwagiliaji (8%).

Kiasi cha mpunga kinachozalishwa nchini kimekuwa kikiongezeka mwaka hadi mwaka kutoka tani 41,000 mwaka 1970 hadi tani 811,500 mwaka 1998. Ongezeko hili limetokana na kuongezeka kwa eneo linalolimwa mpunga na kwa kiasi kutokana na kuongezeka kwa miradi midogo ya umwagiliaji pamoja na matumizi ya teknolojia bora za kilimo.

Maeneo yanayolima mpunga

Maeneo yanayolima mpunga kwa wingi Tanzania ni; Morogoro maeneo ya bonde la kilombero/Ifakara, Dakawa, Malolo; Mbeya: Kyela, Mbarali; Shinyanga: Kahama; Mwanza, Bonde la Ruvu mkoani Pwani. Na maeneo mengine mengi.

shamba-la-mpunga
Sehemu ya shamba la mpunga uliostawi vizuri

pH ya udongo (Soil pH) inayofaa kwa Mpunga

pH ni kipimo kinachoonyesha kiwango cha tindikali au nyongo katika udongo. Udongo waweza kuwa tindikali (ph ndogo kuliko 7), nyongo (ph kubwa kuliko 7), au katikati (neutral) – ph ya 7.

Tindikali au nyongo ya udongo hupimwa kwa kutumia pH mita. Mazao mengi hustawi zaidi katika udongo wenye hali ya tindikali ya wastani (kipimo cha pH 5.5 hadi 7.0).

Mpunga hustawi kwenye udongo wa mfinyanzi wenye tindikali ya wastani na virutubisho vya kutosha.



Maandalizi ya shamba la Mpunga

Ni vyema mashamba yaandaliwe mapema kabla ya msimu wa kupanda haujaanza ili kumpa mkulima fursa ya kupanda kwa wakati unaotakiwa. Kuna njia mbalimbali zinazotumika kuandaa mashamba. Kati ya njia hizi ni pamoja na kufyeka, kung’oa visiki na kulima. Shamba linaweza kulimwa kwa kutumia:

  • Jembe la mkono – wengi wanatumia
  • Jembe la kukokotwa na wanyama kama ng’ombe
  • Power tillers
  • Matrekta

Baaada ya kulima, shamba linawekwa maji ili liloane vizuri na kisha udongo unachanganywa vizuri na maji ili kutengeneza tope. Hii inafanyika kwa kuvuruga au kuchavanga (puddling). Hii inarahisisha kupandikiza miche na kuhifadhi maji.

Sasa unaweza kujipatia Kitabu (PDF) cha Mwongozo wa kilimo cha Mpunga sasa hivi kwa bei nafuu sana. Kitabu hiki kimeboreshwa zaidi kwa ushauri wa kitaalam, mapendekezo ya kiasi, na aina za mbegu bora, mbolea na viuatilifu vya kutumia pamoja na mchanganuo wa bajeti ya kilimo na faida. Bofya hapa kukipata ndani ya Whatsapp au bofya hapa kukipata kwa email.


Aina za Mbegu za Mpunga

Matumizi ya mbegu bora ni muhimu katika upatikanaji wa mavuno mengi na bora. Kuna makundi mawili makuu ya mbegu za mpunga ambayo ni:

1. Mbegu za asili za mpunga

Ni zile ambazo zimetumika miaka mingi katika historia ya kilimo. Kuna aina nyingi za mipunga ya asili inayolimwa sehemu mbalimbali hapa nchini kama Supa, Kahogo, Kula na Bwana, Shingo ya mwali, n.k.

Wakulima wanazipenda mbegu hizi kutokana na kuwa na sifa kama vile ladha nzuri, uvumilivu wa matatizo mbalimbali ya kimazingira na kwa sababu ya uwezo wa mbegu hizi kustahimili katika hali mbaya ya hewa na hazihitaji uangalizi wa hali ya juu. 

Sifa hizi ni matokeo ya mbegu hizi kumudu mazingira na uchaguzi wa mbegu uliofanywa na wakulima kwa miaka mingi. Hata hivyo, nyingi ya mbegu hizi zina uwezo mdogo wa kuzaa, zinachelewa kukomaa, ni ndefu na rahisi kuanguka.

2. Mbegu bora za mpunga

Hizi ni zile zilizoboreshwa kutokana na mbegu za asili. Mfano wa mbegu za mpunga zilizoboreshwa ni kama vile Katrin, IR54, na IR64. Zinazaa sana hasa kwa kilimo cha umwagiliaji.

Hata hivyo, hazikidhi ladha ya walaji na ukobolekaji wake si mzuri na baadhi hazistahimili kwenye mazingira mengi ya kawaida. Hii imezifanya mbegu hizi kukubalika na wakulima kwa kiwango kidogo sana. 

Mbegu bora nyingine zilizozalishwa kutoka utafiti na kuonekana kupendwa kwa ajili ya mavuno mengi na ladha nzuri ni kama TXD88 na TXD85.

Mbegu ya SARO 5 (TXD306)

Hivi karibuni imetolewa mbegu nyingine inayoitwa TXD306 au kwa jina maarufu SARO 5. Mbegu hii ya mpunga inapendwa sana na wakulima, wafanyabiashara na walaji.

Hii ni kutokana na sifa yake ya kutoa mavuno mavuno mengi, punje ndefu kiasi na nzito, ladha nzuri na yenye kunukia pindi ipikwapo na kuliwa.

Mbolea za kupandia mpunga

Mbolea zinazofaa kupandia mpunga ni zile zenye kirutubisho cha P (phosphate), ambazo ni kama MAP, DAP au Minjingu Mazao.

Viwango vya mbolea za kupandia

Kiwango cha mbolea za kupandia kinachopendekezwa ni kilo 20 phosphate (P) kwa hekta moja ambayo ni sawa sawa na mifuko mitatu ya DAP kwa hekta (= mfuko mmoja kwa ekari).

Hii ni sawa na mifuko miwili kwa hekta ya Minjingu Phosphate (= mfuko mmoja na nusu kwa ekari) au mifuko minne na nusu kwa hekta ya Minjingu Mazao (= mifuko miwili kwa ekari).

Wakati wa kuweka mbolea za kupandia

Mbolea ya kupandia mpunga iwekwe kabla ya kupanda mbegu za mpunga au kupandikiza miche ya mpunga.

Kabla ya kuweka mbolea hakakisha kuwa majaruba yanatengenezwa ili kuhakikisha maji hayaingii na kutoka kiholela. Mbolea ya kupandia mpunga huwekwa kwa kusia katika jaruba kabla ya kuchavanga.

Kuchavanga husaidia kuchanganya udongo na mbolea na pia kutengeneza eneo zuri la kupandikiza miche. Baadaye miche hupandikizwa.


Upandaji wa Mpunga

Njia za upandaji wa mpunga

Kitaalam, kuna njia mbili kuu zinazotumika kupanda mpunga shambani. Njia hizo ni ile ya kupanda mbegu moja kwa moja na ile ya kupandikiza miche.

1. Kupanda mbegu moja kwa moja

Njia hii hutumika kwa kupanda mbegu za mpunga moja kwa moja kwenye shamba lililotayarishwa vizuri. Njia ya kawaida (ya kienyeji) wanayoitumia wakulima ni ile ya kumwaga kwa kuzitawanya mbegu (yaani broadcasting) na kuzifukia mbegu.

Njia ya kitaalam ni ile ya kupanda mbegu kwenye mashimo yaliyo kwenye mistari na kwa kuzingatia nafasi maalum. Lakini pia mbegu zinaweza kupandwa kwenye mashimo yaliyoandaliwa bila kufuata mstari wala kuzingatia nafasi iliyopendekezwa (dibbling).

Vile vile mbegu za mpunga huweza kupandwa kwa kunyunyizwa kwenye vifereji vyenye vina vifupi na kufukiwa pasipo kuwa na nafasi maalum kati ya punje na punje (seed drilling).

2. Kupandikiza miche ya mpunga

Njia hii hutumika kwa kupanda mbegu kwanza kwenye kitalu kabla ya kuzihamishia shambani. Mara nyingi mbegu za mpunga hutumia wiki mbili hadi tatu baada ya kuota kwenye kitalu ili kufikia umri wa kupandikizwa shambani.

Katika shamba, miche ya mpunga huweza kupandikizwa kwa kufuata mistari na kwa nafasi maalum au kwa kufuata mistari tu bila nafasi maalum au kupandikizwa kiholela bila kuzingatia nafasi maalum za kupandia.

Inashauriwa kupandikiza miche katika kina cha sentimeta 2 hadi 3. Ukipanda kina kirefu machipukizi huchelewa kujitokeza. Baada ya kupandikiza miche, machipukizi hujitokeza baada ya siku 5 hadi 10.

Kupandikiza-mpunga
Kupandikiza miche ya Mpunga

Nafasi ya kupanda mpunga

Kama unatumia mbegu za asili, panda mpunga kwa kutumia nafasi ya sm 20 kwa sm 20 au sm 25 kwa sm 25 au sm 30 kwa sm 30.

Na ikiwa unatumia mbegu bora inashauriwa kutumia nafasi ya sm 15 kwa sm 15 au sm 20 kwa sm 20.

Kwenye mpangilio wa mistari miwili miwili (double rows), nafasi kati ya mistari miwili ni sm 10, na nafasi kati ya mimea katika kila mstari ni sm 20, na nafasi kati ya mistari miwili na mistari miwili mingine (double rows) ni sm 40.

Kupanda kwa nafasi ni kati ya njia bora za kilimo inayomwezesha mkulima kupata mazao bora. Hivyo ni muhimu sana kuzingatia kupanda kwa mistari na kufuata nafasi zinazoshauriwa na wataalamu wa kilimo.


Wakati kupanda Mpunga

Muda wa kupanda unatofautiana kutoka eneo moja hadi jingine kulingana na majira ya mvua.

Kwa mfano katika wilaya ya Morogoro tarehe za kupanda ni kuanzia Desemba hadi Januari kwa mpunga wa muda mrefu.

Kwa mpunga wa muda wa kati na muda mfupi, tarehe za kupanda ni Februari hadi Machi.

Kupalilia Mpunga

Ni muhimu shamba lipaliliwe ili kuondoa magugu. Magugu ni mimea hivyo hushindana na mimea iliyopandwa na mkulima kwa kunyonya virutubisho ardhini. Magugu yanaweza pia kuhifadhi wadudu na magonjwa yanayoweza kushambulia mimea iliyopandwa na hivyo kupunguza mavuno.

Katika kilimo cha mpunga, ni muhimu shamba lipaliliwe siku 14 hadi 21 baada ya mimea kuota kufuatana na hali ya shamba wakati wa kupanda. Ni vizuri katika kilimo cha mpunga, shamba lipaliliwe mara mbili, kutegemeana na hali ya magugu katika shamba. Unaweza kupalilia kwa kung’olea kwa mkono, kwa mashine au kwa kutumua viua magugu (herbicides) kama vile 2, 4-D (Two Four D).

Utafiti unaonyesha kwamba, shamba la mpunga ambalo halijapaliliwa linaweza kupunguza mavuno kwa asilimia 60 hadi 100 ya mavuno yanayotarajiwa. Hata kama mkulima atatumia mbegu bora, aina na kiasi cha mbolea zinazoshauriwa, kupanda kwa mstari pamoja na mbinu nyingine bora zinazoshauriwa, bila kupalilia hali hii itaathiri mavuno yake.


Mbolea za kukuzia mpunga

Ni mbolea zinazotumika baada ya mimea kuota kwa lengo la kuikuza mimea ili itoe mavuno bora. Mara nyingi mbolea hizi zinatoa kirutubisho cha naitrojeni. Kiwango kinachopendekezwa ni kilo 60 naitrogeni kwa hektari, ambacho ni sawasawa na kiasi cha mifuko miwili ya UREA au Minne na Nusu Ya CAN au Mitatu ya SA. Mbolea inayotumika mara kwa mara ni Urea. Hata hivyo mbolea zingine kama SA inaweza kutumika kama kuna mahitaji ya salfa. CAN inaweza kutumika kama kuna mahitaji maalum ya nitrate na ammonium. Kwenye mpunga, mbolea ya kukuzia inawekwa wiki mbili baada ya kupandikiza miche na irudie tena baada ya wiki nne.

Kuweka mbolea: Mbolea ya kukuzia hutiwa kwa kusia wiki mbili baada ya kupandikiza, na kurudia mwezi mmoja baadaye. Ni vyema kuweka mbolea za kukuzia mara mbili ya kiasi kinachopendekezwa.

Shamba-la-Mpunga-uliopandikizwa
Shamba la mpunga uliopandwa kwa mistari

Kudhibiti Magonjwa na Wadudu Wanaoshambulia Mpunga

Magonjwa Yanayoshambulia Mpunga

Magonjwa ya mpunga yamegawanyika katika makundi matatu kulingana na vimelea visababishi ambavyo ni fungasi, virusi na bakteria.

i) Rice blast (Ukungu)

Unaosababishwa na Pyricularia oryzae.

Dawa/Kudhibiti: Mbegu bora inayostahimili ugonjwa, kupanda mapema, kung’oa mimea iliyoathirika ama kunyunyiza dawa za kuua ‘vectors’ kama vile inzi weupe (white flies).

ii) Brown leaf spot

Unaosababishwa na Helminthosporium spp.

Dawa/Kudhibiti: Panda mbegu kwa udongo unaofaa, weka mbolea ya kuzuia au tibu mbegu na dawa.

iii) Sheath rot

Unaosababishwa na Acrocylindrium oryzae.

Dawa/Kudhibiti: Kwa sasa hakuna njia ya kuzuia

iv) Rice Yellow Mottle Virus (RYMV) – Kimnyanga

Hivi karibuni ugonjwa wa kimyanga umetajwa kama ugonjwa hatari sana kwa mpunga hapa Tanzania.

Dawa/Kudhibiti: Panda mbegu zilizoboreshwa, zinazostahimili magonjwa au ng’oa mimea iliyoathirika.

Magonjwa yasababishwayo na bakteria nayo wametajwa kuwa na madhara makubwa kwa uzalishaji wa mpunga hapa nchini. Bakteria hawa wanajumuisha Acidovorax avenae subsp. Avenae asababishae ugonjwa wa bacterial stripe, Pantoea aglomerans, asababishae ugonjwa wa palea browning na Xanthomonas oryzae p.v. oryzae.


Wadudu wanaoshambulia mpunga

Kuna aina nyingi sana za wadudu wanaoathiri mpunga katika hatua mbalimbali za ukuaji wa mpunga. Wanapokithiri na wasipodhibitiwa hupunguza kiasi cha mavuno shambani.

i) White flies (Funza weupe)

Dawa/Kudhibiti: Nyunyiza dawa ya Thiodan, Endosulfan (Thionex), Fipronil (k.m. Regent 3G), Fenthion (k.m. Lebaycid)

ii) Rice stalk borer waharibifu

Kudhibiti: Nyunyiza dawa ya Thiodan, Endosulfan (Thionex), Fipronil (k.m. Re­gent 3G), Fenthion (k.m. Lebaycid) Ili mkulima aweze kupata mazao mengi na bora inashauriwa kutumia dawa za kuzuia magonjwa na wadudu wanaoshambulia mimea na njia zinginezo.


Kuvuna, Kukausha, Kusafisha na Kuhifadhi Mpunga

Kuvuna: Mpunga uko tayari kuvuna wakati asilimia themanini (80%) ya rangi ya mpunga kwenye masuke imebadilika na kuwa dhahabu. Mpunga unavunwa kwa kukata bua pamoja na suke lake.

Kuvuna-mpunga-kwa-siko

Uvunaji wa mpunga

Kukausha: Rundika pahali pakavu k.m. kwenye tuta la jaruba halafu pigapiga (thresh) ili kutenganisha masuke na mpunga. Kama mpunga hayajakauka vizuri hukaushwa zaidi juani kwa siku 3-4 ili kupunguza unyevunyevu kufikia kiwango kinachofaa kwa kuhifadhi (14%). Ni muhimu mpunga ukauke vizuri ili usioze ukiwekwa ghalani.

Kusafisha: Mpunga uliyokauka vizuri hupepetwa na vilevile mapepe huondolewa. 

Kuhifadhi: Mpunga safi huwekwa kwenye gunia na magunia kupangwa vizuri ghalani juu ya mbao yasiguse sakafu.

Sasa unaweza kujipatia Kitabu (PDF) cha Mwongozo wa kilimo cha Mpunga sasa hivi kwa bei nafuu sana. Kitabu hiki kimeboreshwa zaidi kwa ushauri wa kitaalam, mapendekezo ya kiasi, na aina za mbegu bora, mbolea na viuatilifu vya kutumia pamoja na mchanganuo wa bajeti ya kilimo na faida. Bofya hapa kukipata ndani ya Whatsapp au bofya hapa kukipata kwa email.

Usipitwe na…

Acha comment yako hapa chini ili ku-share mawazo na wakulima wenzetu.

Pls share this post

Farming Tips and Tricks

If you like farming you will definitely love our contents. Join us now

119 Comments

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

  1. Nimefurahi kwa maelezo mazuri ya namna ya kulima mpunga. Nipo na andaa shamba, maelezo yamenipa mwongozo mzuri

  2. Toka mwaka jana nilianza kujihusisha na kilimo cha mpunga na sikupata mazao kutokana na kutokujua ratiba na muda gani wa kupanda na aina gani ya mbegu inatakiwa kupandwa na kwa muda gani. na mwezi huu wa kumi na moja 2018 nitaenda tena morogoro kufatilia mashamba naomba kuelekezwa je ni muda sahihi huu wa kuanza kulima maana safari hii nataka kulima kitalamu yaani mpunga wa kupandikiza,naomba msaada jamani.

    • Mr Elisha huu ni muda sahihi Kwa Mpunga. Unachotakiwa ni kuanza shughuri za kuandaa kitalu na shamba. Unaweza pia kujipatia muongozo wetu wa kilimo cha Mpunga ili ujue hatua site za utunzaji wa Mpunga na gharama zake.

  3. Mr Elisha huu ni muda sahihi Kwa Mpunga. Unachotakiwa ni kuanza shughuri za kuandaa kitalu na shamba. Unaweza pia kujipatia muongozo wetu wa kilimo cha Mpunga ili ujue hatua site za utunzaji wa Mpunga na gharama zake.

    • Unapoona magugu yanakua kwa kasi kuliko unavyoweza kudhibiti. Mwezi mmoja baada ya kupandikiza mpunga, unaweza kupiga dawa ingawa unatakiwa uzingatie pia kasi ya ukuaji wa magugu kwenye shamba lako

  4. Nahitaji kulima mpunga lkn pia nimepata maelezo yenye ufumbuz ktk nililo kuwa nataka kulifanya lkn ,naomba msaada nimbegu ipi ambayo no nzur kwa kipato nahata kibiashara:?

  5. Asante kwa somo sasa kama eneo la kilimo kuna wale ndege wanaoshambulia mpunga.njia ipi ni bora ya kuwaondosha?

    • Gharama anazopitia mkulima ni nyingi lakini pia hazifanani kati ya mkulima mmoja na mwingine. Nashauri upate Muongozo wa Kilimo cha Mpunga ili upate kujua mchanganuo mzima wa gharama zote za uzalishaji na faida tarajiwa ili uweze kupata picha kamili. Tafadhali, wasiliana nami kwa namba 0655570084

  6. uwekaji wa mbolea ya kupandia kwenye zao la mpunga bado ni changamoto,kuweka kabla ya kuchavanga mbolea nyingi hupotea. naomba ushauri wako

  7. Bwana Mtalula hongera sana kwa maelezo mazuri ,Mungu akubariki sana elimu uliyotoa.
    Samahani ningependa kujua ni wakati gani wafaa kupanda mpunga Ukanda wa Pwani?na kwa mbegu gani?

  8. Kuna dawa ya kiua gugu aina ya RICEBAC
    na .
    Nominee gold
    Naomba kujua ubora wa dawa kati ya hizi mbili viua gugu Kafka mpunga

  9. Hello, habari! Mimi swali langu ni tofauti na kilimo. Nimefanya majaribio ya kilimo cha lozera, naomba nijue kama unaweza kunisaidia elimu yake. Maana kwny mitandao elimu ni finyu mno.

  10. Hàbari, ningependa kufahamu juu ya mpunga baada ya kuvuna inahitajika ûanikwe kwa muda gani kabla ya kwenda kukobolewa?

  11. Habari Mimi ninaomba kijua mpunga wa kupanda punje je unawekwa mbolea ya kukuzia
    baada ya mda gani toka kuota na baada ya hsapo naludia Tena baada ya mda gani na mbolea ya kuzalishia naweka baada ya muda gani???

  12. Naomba namba ya simu ili niwasiliane na ninyinyi kwa sababu nataka mbegu ya supa na kahogo niko Mbeya nalimia usangu.

    • Pia ninatamani kutumia mkojo wa Sungura je unaweza kunipa elimu ya matumizi ya mkojo wa sungura kwa kilimo cha Mpungu na Mahindi

    • Habari kaka

      Mimi ni mfanyi biashara kutoka Mombasa Kenya, nataka kununua mpunga laini( chakula cha mifugo) Naeza kununua zaidi ya tani mia moja kwa mwezi… nataka kufanya biashara ya kuendelea. Ikiwa inaezekana Naomba unijulishe.+254 722 777058.
      Asante sana

  13. Ninaomba darasa hili liwe endelevu kama mnavyojua wakulima wengi tunalima kwa mazoea ni idara inayohitaji mafunzo zaidi ili kulima kibiashara.

  14. Habari zenu nimefray sana kwa mafundisho naomba niache namba zangu maana naitaji sana tena sana kuona na nyinyi na vitabu pia na elimu nyingine 0682 394025 0742060678

  15. Je! Kwenye mpunga hauhitaji mbolea ya kuzalishia? Na ni kiasi gani na ni aina gani km unalima maeneo ya Ifakara?

  16. Andiko zuri. Ila viuatilifu ambavyo haviruhusiwi usingeviweka kwenye andiko lako. Mathalani matumizi ya Thiodan.

  17. hivi kwa tanzania hi kuna megu za mpunga ambazo zinaweza kustahimili ukame? au za kupandwa sehemu ya kawaida kama mahindi?

  18. Asante saana kwa doze ,, naomba uandike majina ya viuatilifu vilivyopo sokoni ,, pia ujue wanaosoma andiko lako sio wataaluma wa kilimo ! Asante saana kwa kutumia lugha nyepesi

  19. Kilimo ni uti wa mgongo kwa wakulima nipo geita napata wap mbegu za kisasa za mda mfupi nisaidie pia

  20. Nimebarikiwa sana na maelekezo yenu kuhusu namna ya kulima mpunga kisasa. Mwaka huu Mungu akiruhusu, nitafuata kanuni hizo. Asanteni sana.

  21. Shukran sana kaka kwa ufafanuzi mzuri, naamini kwa kufuata haya maelekezo wengi tuta overcome changamoto za kupata mazao kidogo kwenye kilimo cha mpunga, Mungu akubariki.

  22. 💝☑️
    Mbona nlicherewa kujua huku jaman na hamsemi ata kule TBC???
    I have learned something new
    H
    Thanks 👍